Warsha Ya Mapitio Ya Mitaala Nchini

Serikali imedhamiria kufanya mapitio na kuhuisha
mitaala katika Vyuo vya elimu ya juu kupitia Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi
ya Kiuchumi (HEET), ili wataalam watakapohitimu masomo wawe na uwezo wa
kujiajiri na kukidhi mahitaji ya soko la ajira.
Hayo yamesemwa na Kaimu Mkuu wa Chuo cha Uhasibu
Arusha (IAA), Dkt. Cairo Mwaitete wakati akimwakilisha Katibu Mkuu Wizara ya
Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Francis Michael, katika ufunguzi wa Warsha
ya siku nne ya Mapitio ya Mitaala ya Vyuo vya Elimu ya Juu,
inayofanyika katika Chuo cha Uhasibu Arusha.
Amesema
warsha hii imewakusanya wataalam kutoka Vyuo mbalimbali vya elimu ya Juu hapa
nchini kujadili namna bora ya kufanya
mabadiliko ya mitaala ambayo ipo katika vyuo vyao, ili mitaala hii
itakapoandaliwa vijana waweze kuajiriwa na kujiajiri wenyewe na kutumia
rasilimali zilizopo katika mageuzi ya kiuchumi.
“
Vijana wengi wa vyuo vyuo vya elimu ya juu wanajifunza lakini wanashindwa
kuajirika, hivyo ipo haja ya kupitia upya mitaala, hata Rais wetu Mhe. Dkt.
Samia Suluhu Hassan alitoa maelekezo kupitia Wizara ya Elimu kwamba kuwe na
mapitio, ambayo itawafanya vijana waweze kuajirika na kujiajiri pia,”
alisisitiza Dkt. Mwaitete.
Mratibu
Msaidizi wa Mradi wa HEET, Dkt. Evaristo Mtitu amesema kupitia mradi huu
taasisi za elimu ya juu zinaenda kuhuisha mitaala iliypopo na kuunda mitaala
mipya ili kutoa nafasi kwa wanafunzi wanaosoma mitaala hiyo kupata elimu ujuzi
na stadi za maisha za kukabiliana na mazingira popote ndani na nje ya nchi.
Ameongeza
kuwa mradi huu utatekelezwa kwa miaka mitano huku malengo yakiwa ni kujenga na
kukarabati miundombinu, kusomesha wanataaluma (Shahada ya Uzamili na Uzamivu),
kuimarisha matumizi ya TEHAMA na kupitia mitaala iliyopo na kuunda mitaala
mipya kwenye maeneo ya kipaumbele ya nchi ili ijielekeze katika kutoa elimu
ujuzi.
Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi
(HEET) unafadhiliwa na Benki ya Dunia kwa thamani ya dola za Kimarekani milioni 425 kwenye vyuo vyote vikuu vya
Serikali , vyuo vitano ambayo viko chini ya Wizara ya Fedha na Mipango pamoja na taasisi ambazo zinasaidia
uendeshaji wa elimu ya juu nchini, zikiwemo Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu,
Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) na Tume
ya Sayansi.