Mahafali Ya 24 Chuo Cha Uhasibu Arusha IAA

Mkaguzi
mkuu wa Ndani wa serikali Bw. Athuman Mbuttuka
ameupongeza uongozi wa Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA) kwa kuanzisha
mafunzo ya uanagenzi (apprenticeship) katika fani za utalii, fedha na bima,
yatakayowawezesha wahitimu kupata ujuzi
na utaalam kutoka kwenye soko na kumudu mahitaji ya soko, kijamii na kiuchumi.
Mbuttuka
ameyasema hayo leo tarehe 16 Desemba katika mahafali ya 24 ya Chuo Cha Uhasibu
Arusha yaliyofanyika katika ukumbi wa AICC Arusha, ambapo amewatunuku
astashada, stashahada, Shahada na Shahada za Uzamili katika fani mbalimbali
akimwakilisha Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Mwigulu Nchemba.
“Ni
matumaini yangu kuwa vyuo vingine nchini vitaiga mfano huu mzuri katika
kuboresha mitaala yao, ili Taifa liwe na wahitimu wenye stadi shindani watakaokabiliana
vema na mahitaji ya kijamii na kiuchumi ya sasa,” alisema Mbuttuka.
Aidha, Mbuttuka ametoa rai kwa vyuo vyote
nchini kuhuisha mitaala yao katika fani za biashara na uongozi kuhakikisha fani
hizo zinajumuisha stadi za TEHAMA na kuweka mkazo kwenye mafunzo ya akili isiyo
asili (artificial intelligence), ili wahitimu wa fani za biashara, uhasibu na
ukaguzi wawe na stadi zinazohitajika katika soko la dunia ya leo.
Mwenyekiti
wa Baraza la Uongozi wa Chuo-IAA, Dkt.Mwamini Tulli amesema kumekuwa na
ongezeko la wahitimu kutoka 2,481 mwaka 2020/2021 mpaka 3529 mwaka
2021/2022, huku akiwaasaa wahitimu kuondokana na dhana ya kuajiriwa pekee
badala yake wajiamini kutumia elimu waliyopata katika kupambana na maisha.
Naye
Kaimu Mkuu wa Chuo IAA, Dkt. Cairo Mwaitete amemshukuru Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kukiwezesha Chuo kupata
fedha za Mradi wa HEET kiasi cha shilingi bilioni 44 kwa ajili kuboresha
miundombinu, kuboresha na kuhuisha mitaala na kuwaendeleza watumishi kuelimu.
Dkt.
Mwaitete ameongeza kuwa kutokana na uboreshwaji wa miundombinu unaoendelea
kupitia fedha za ndani, kumekuwa na
ongezeko la idadi ya wanafunzi kutoka 3000 katika mwaka wa masomo 2017/18
kufikia wanafunzi zaidi ya 13,000 mwaka 2022/23.
Stanslaus
Ismail mwakilishi wa Wahitimu wa masomo ya Shahada ya Uzamili, ameushukuru
uongozi wa IAA kuhakikisha wanakuwa mahiri katika utafiti, kuimarisha
miundombinu ya TEHAMA iliyowawezesha kusoma, kufanya mitihani huku akibainisha
namna walivyoandaliwa kujiajiri kupitia Kiotamizi (Business Start Up Center).
Jumla ya wahitimu 3529 wametunukiwa astashada,
stashahada, Shahada na Shahada za Uzamili katika mahafali ya 24 ya Chuo Cha
Uhasibu Arusha iliyofanyika katika ukumbi wa AICC Arusha.